Naibu Waziri wa Madini, Prof. Shukrani Manya akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini ya Almasi katika Kijiji cha Mwanh'olo wilayani Kishapu ambao wanaodaiwa kuvamia eneo la mwekezaji, Mgodi wa Al-Hilal
Wachimbaji wadogo wa madini ya Almasi waliovamia na kuanza kuchimba katika kijiji cha Mwanh'olo kata ya Mwadui Lohumbo wilayani Kishapu mkoani Shinyanga wamepewa siku mbili wawe wameshaondoka eneo hilo kwa hiari ili kumpisha mwekezaji mwenye leseni aendelee kufanya shughuli zake katika eneo hilo.
Agizo hilo limetolewa leo Januari 21, 2021 na Naibu Waziri wa Madini, Prof. Shukrani Manya, wakati akiwa kwenye ziara yake ya siku moja mkoani humo, ambapo alizungumza na wanunuzi wa madini na viongozi wa chama cha wachimbaji (SHIREMA) pamoja na wachimbaji wadogo wanaochimba katika kijiji cha Mwanh’olo kata ya Mwadui Lohumbo wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.
Manya amesema serikali ya awamu ya tano inawapenda wananchi wake na inataka waweze kupata maendeleo yao wenyewe na Taifa kwa ujumla, hivyo inawaomba wachimbaji hao waweze kuondoka katika eneo hilo kwa sababu ni eneo la mwekezaji Al-Hilal ambaye tayari analeseni yake, wao watatafutiwa eneo lingine ili waweze kuendelea na shughuli za uchimbaji.
"Nawaombeni sana muwe wasikivu na muweze kuelewa vizuri huu ujumbe wa serikali niliouleta kwenu, kwa sababu serikali inawapenda, hivyo inawapa siku mbili mkusanye mchanga wenu mliouandaa jiungeni kwenye vikundi muwe na leseni yenu, serikali itawatafutia eneo zuri ambalo mtaendelea kuchimba bila kuwa na migogoro na yeyote, kinachotakiwa muwe waaminifu mnapopata mali muuzie katika soko letu na serikali iweze kuingiza kipato," amesema Manya.
Naibu waziri Manya amesema eneo hilo siyo shamba la mtu kama wanavyojua ni mali ya serikali ambayo imeshakatiwa leseni na mwekezaji Hamad Hilal, hivyo wanatakiwa watoke kwa hiari kwani watatafutiwa eneo lingine la kuchimba ili mwenye leseni yake aendelee kufanya shughuli zake za uchimbaji.
Baadhi ya wachimbaji wadogo wanaochimba katika eneo hilo Zainabu Said na Reonald Daudi walisema wamekubali kuondoka ila wanaomba wapewe muda wa wiki moja ili waweze kuosha mchanga wao kwa sababu muda waliopewa ni mdogo sana na kuiomba serikali kuwatafutia eneo linguine la uchimbaji ili waweze kuendelea na shughuli hiyo.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainabu Telack akitoa taarifa kwa naibu waziri Manya amesema anashukuru kwa kufika Naibu Waziri huyo, hivyo anaamini atasaidia kuondoa mgogoro baina ya wachimbaji wadogo na mwekezaji Al-Hilal, maana tayari nae alikuwa na mpango wa kuwapa siku chache wawe wamedhaondoka eneo hilo
"Mimi na kamati yangu ya usalama wa madini tukishirikiana na Halmashauri ya wilaya ya Kishapu tulishakuja katika kijij hiki na kusitisha uchimbaji, tunaomba mtii sheria na" amesema Terack.
Naye afisa Madini wa mkoa wa Shinyanga Joseph Kumburu amesema tayari ofisi ya madini April 20, 2020 ilishawatoa wachimbaji 400 ambao walivamia eneo hilo lakini wakaja kurudi tena na sasa lina wachimbaji zaidi ya 1000 hivyo ofisi ya madini ilikuwa inajiandaa jinsi ya kuwaondoa na kuwakamata wachimbaji wanaovamia katika eneo la muwekezaji Al-Hilal, na kuwakamata wale wanaojimilikisha maeneo hayo.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa