Waziri wa mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amepiga marufuku Halmashauri zote nchini kutumia wafanyabiashara kuchanja mifugo na kutaka kuvunjwa kwa mikataba hiyo.
Waziri Ndaki amesema hayo alipofanya ziara ya kikazi katika wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga Desemba 31, 2020 na kutembelea josho la kuogeshea mifugo katika kata ya Mipa wilayani Kishapu.
“Halmashauri zetu zote kuanzia leo ni marufuku kutumia wafanyabiashara kuchanja mifugo yetu, halmashauri zitumie wataalamu kupitia wizara ambao wamethibitishwa waweze kuchanja mifugo ya wananchi wetu.” Alisema Ndaki.
Waziri Ndaki ametoa maagizo hayo baada ya kupata malalamiko kutoka kwa wafugaji kuhusu kuvimba kwa ng’ombe inayochangiwa na chanjo hizo.
“Hao wafanyabiashara kama mmeingia nao mkataba, ivunjeni haraka iwezekenavyo, hatuwezi kutumia wfanyabiashara kuchanja ng’ombe halafu wanavimba halafu taarifa hatuna. Hawa wafanyabiashara wapo kibiashara zaidi” aliongeza Ndaki.
Hata hivyo, alipata fursa ya kuongea na wafanyabiashara na wafugaji katika mnada wa upili wa Mhunze uliopo wilayani Kishapu ambapo aliweza kusikiliza kero zao ikiwemo ya kuchelewa kuondoka mnadani hapo mara baada ya kumaliza kufanya biashara hadi ifikapo sa 12 jioni hali inayohatarisha maisha yao. Walisema muda huo kuna fisi kwenye mashamba hali iliyomlazimu waziri kuutaka uongozi wa mnada huo utafute utaratibu wa kuwaruhusu wafanya biashara kuondoka mara tu baada ya kumaliza biashara zao.
Wilaya ya Kishapu ina idadi ya mifugo ipatayo 232,569 wakiwemo ng’ombe, mbuzi, kondoo kuku na bata. Kwa kutumia mradi wa kujengea wanajamii uwezo kwa kutumia mfumo wa ekolojia ambapo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 mradi umetekelezwa ambapo umeanzishwa ujenzi wa kiwanda kidogo cha ngozi kijiji cha Kiloleli chenye thamani ya shilingi milioni 95, kuanzisha kituo cha unenepeshaji wa mifugo kijiji cha Muguda wenye thamani ya shilingi milioni 107, ujenzi wa josho la kuogeshea mifugo katika kijiji cha Mihama wenye thamani ya shilingi milioni 40, ujenzi wa marando katika kijiji cha Kiloleli wenye thamani ya shilingi milioni 13.
Hata hivyo halmashauri imetenga eneo la kulishia mifugo ambalo ni takribani hekari 115 katika vijiji vinne wilayni Kishapu. Hii inawasaidia wafugaji kupata mifugo bora kwa ajili ya ushindani wa soko.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa