Madiwani wa halmashauri ya Kishapu mkoani Shinyanga wamempongeza mkurugenzi wa halmashauri ya Kishapu Emmanuel Johnson kwa utendaji na utekelezaji wa ufanisi na weledi wa kuweza kusimamia mapato ya ndani, ambapo amekusanya zaidi ya sh 2 bilioni sawa na asilimia 92.2 .
Ambapo makusanyo ya bajeti ya mwaka ni zaidi ya sh 3 bilioni, na fedha hiyo imekusanywa kuanzia julai 2022 hadi Mei 10, 2023 sawa na asilimia 92.2 ya makisio ya bajeti.
Akitoa pongezi hizo diwani wa kata ya Seke Bugolo Ferdinand Mpogomi kwa niaba ya mwenyekiti wa halmashauri hiyo leo jumatano Mei 10, 2023 kwenye kikao cha baraza la madiwani lililofanyika katika ukumbi wa halmashauri hiyo, amesema makusanyo haya yameiwezesha halmashauri kutekeleza miradi yake mbalimbali ya maendeleo.
"Makusanyo haya pia yamesaidia ujenzi wa kituo cha afya kwa gharama ya Sh 500 milioni, na ujenzi upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji, hivyo tumuombe mkurugenzi aendelee kuongeza kasi zaidi kwa kushirikiana na watendaji wake ili kuhakikisha anakusanya mapato zaidi, na sisi tutaendelea kusimamia ipasavyo,"amesema Mpogomi.
Mpogomi amesema usimamizi bora wa mapato na matumizi ya fedha za serikali umesaidia halmashauri kupata hati safi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, na ukamilishaji wa miradi ya maendekeo kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo William Jijimya amesema leo madiwani wamempongeza mkurugenzi, hivyo ameomba pongezi hizo zikazae matunda mengine, ukusanyaji ukaongezeke zaidi na utekelezaji ili kuhakikisha halmashauri inakuwa na maendeleo kama halmashauri zingine.
"Kwenye ukweli tuseme ukweli kwa sasa tuko kwenye asilimia 92, hivyo tunaenda kufunga mwaka kwa asilimia zaidi ya 100, kwa kuwa na asilimia hii tusipunguze kasi na mtumishi akifanya vizuri anapewa pongezi ili aendelee kupiga kazi na kuijenga halmashauri yetu ya Kishapu,"amesema Mwenyekiti William Jijimya
Aidha mkuu wa wilaya ya Kishapu Joseph Mkude amewataka madiwani na watendaji kushirikiana vizuri ili waweze kufanya kazi nzuri na kusimamia ipasavyo fedha zinazoletwa na Rais Samia Suluhu za kutekeleza miradi mbalimbali ya kimaendeleo.
"Niwaombe tena tuwe na ushirikiano mkubwa na sifa yetu iendelee, tusiruhusu migogoro iingie katika sehemu za kazi,niwaombe madiwani tusimamie majukumu yetu pale watendaji wanapofanya kazi tunatakiwa tuendelee kusimamia na kuzingatia uongozi wa utawala bora,"amesema Mkude.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Mang'era Marwa amesema wataendelea kufanya kazi kwa bidii kama maagizo yalivyotolewa, ili kuhakikisha halmashauri inakuwa na maendeleo na kuvuka kiwango cha makisio ya bajeti iliyopo.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa