Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Mhe. Joseph Modest Mkude amefanya ziara ya kutembelea miradi ya maji katika kata ya Bupigi na Bubiki inayotekelezwa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kwa ajili ya kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi ili kuboresha hali ya maisha.
Mkude amefanya ziara hiyo leo Jumatano Septemba 14,2022 akiwa ameambatana na maafisa wa RUWASA wakiongozwa na Meneja wa RUWASA wilaya ya Kishapu Mhandisi Dickson Kamazima.
Miradi aliyotembelea ni pamoja na mradi wa Maji ya Bomba ambacho chanzo chake ni Kisima kirefu wa Mwamishoni - Nyasamba katika kata ya Bubiki uliojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 967 (Tsh. 967,811,515/=) pamoja na Mradi wa maji ya bomba ambao chanzo chake ni Ziwa Victoria wa Bupigi - Butungwa katika kata ya Bupigi unaojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 499 (Tsh. 499,514,650/=.
Akizungumza katika ziara hiyo, Mkude amesema lengo la serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salamba pamoja na kumtua mama ndoo kichwani na kumpunguzia umbali wa kwenda kutafuta maji na badala yake kumuongezea muda wa kufanya shughuli zingine za maendeleo ili kujiimarisha kiuchumi na kijamii.
Mkude ameipongeza RUWASA Kishapu kwa kusimamia vizuri mradi wa maji wa Mwamishoni - Nyasamba na kuhakikisha wanatumia vizuri fedha zilizotolewa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi sambamba na kumtua mama ndoo kichwani.
"Nawapongeza Mkandarasi anayetekeleza mradi huu pamoja na RUWASA kwa usimamizi mzuri, mradi umekuwa na matokeo mazuri. Lengo la Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuleta fedha nyingi ni kutaka kuona fedha zinaleta matokeo makubwa na kuondokana na tatizo la maji...
Licha ya kwamba mradi huu wa maji umeshaanza kuwanufaisha wananchi,wanapata huduma ya maji, Tunachohitaji kuona sasa ni mradi unakamilika mapema, kamilisheni sehemu zilizobaki ikiwemo ujenzi wa fensi ", amesema Mkude.
Mkuu wa wilaya amewataka viongozi wa vijiji pamoja na wananchi kushirikiana kulinda miundombinu ya maji huku akiziagiza Jumuiya za watumiaji maji kukusanya fedha na kutumia fedha kwa ajili ya uendelevu wa mradi wa maji.
"Hongereni kwa kupata maji safi na salama, Jukumu lililobaki sasa ni kutunza miundombinu ya maji. Hiki ni kitu chenu, mmepunguza adha ya kutafuta maji kwa umbali mrefu, tunzeni mradi huu..
"Wilaya ya Kishapu bado inakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji kwani tupo chini ya asilimia 60. Serikali inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ili kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama ndani ya mita 400", ameongeza Mkude.
Akiwa katika mradi wa maji Bupigi - Butungwa, Mkuu huyo wa wilaya ya Kishapu licha ya kushuhudia huduma ya maji ikitolewa, amemtaka Mkandarasi anayetekeleza mradi huo, uliofikia 85%, Bent Company Ltd kukamilisha mradi huo haraka kwa kujenga fensi, chemba na kupaka rangi.
"Nafurahi kuona huduma ya maji imeanza kutolewa lakini Mradi huu unasuasua. Mkandarasi hakikisha unakamilisha mradi huu ndani ya wiki mbili kama ulivyoahidi. Wewe ni ndugu yangu tusiharibiane. Meneja RUWASA nakupongeza kwa kazi nzuri wananchi wanapata maji lakini nataka mradi ukamilike kwa wakati", amesema Mkude.
Naye Meneja wa RUWASA wilaya ya Kishapu,Mhandisi Dickson Kamazima amesema mradi wa maji Bupigi - Butungwa unaojengwa kwa fedha za UVIKO - 19 unatakiwa kukamilika kabla ya Septemba 30,2022 ujenzi wake umefikia 85% ukitarajiwa kuwanufaisha wananchi zaidi ya 2000 ukiwa na vituo vinne vya kuchotea maji huku mradi wa maji Mwamishoni - Nyasamba uliokamilika kwa 90% ukinufaisha wananchi zaidi ya 6500 ukiwa na vituo 13 vya kuchotea maji (DP 6 Nyasamba na Mwamishoni 7).
“Mradi wa maji wa Bupigi – Butungwa ulianza kujengwa Januari 2022 unatarajiwa kukamilika Septemba 2022. Fedha hizi ni ufadhili wa Mpango wa Maendeleo kwa ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO - 19 kutoka serikali kuu”,amesema Mhandisi Kamazima.
Aidha ametumia fursa hiyo kuwaomba wananchi wote kushirikiana kulinda miundombinu ya maji ili kuiwezesha huduma ya maji kuwa endelevu kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho.
Kwa upande wao wananchi akiwemo Magdalena Stephano na Japhet Joseph na Daudi Ndaki wameishukuru serikali kuwapatia huduma ya maji safi na salama wakieleza kuwa ilikuwa changamoto ya muda mrefu walikuwa wanatumia muda mwingi kufuata maji na asilimia kubwa maji machafu kwenye mabwawa, mashimo na mito.
"Changamoto hii ya maji sasa imekwisha..Tumemaliza changamoto ya maji, Mateso yetu ya maji yamefikia kikomo", wamesema.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa