Mwenyekiti wa Kamati ya Uchunguzi wa kuvunjika kingo za Bwawa la Maji Tope katika Mgodi wa uchimbaji madini ya Almasi (Williamson Diamond Limited) uliopo Kishapu Mhe. Joseph Modest Mkude ametembelea Mgodi huo ili kufahamu hatua gani zimechukuliwa tangu Bwawa hilo la Maji Tope lilipobomoka na kuharibu makazi na mashamba ya wananchi wa vijiji vya Ng'wanholo na Nyenze vilivyopo katika Kata ya Mwadui Luhumbo kwa kufunikwa na tope Novemba 7,2022.
Mkude ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Kishapu amefanya ziara hiyo katika Mgodi wa Almasi wa Mwadui leo Jumatatu Januari 23,2023 akiwa ameambatana na Wajumbe wa kamati ya Usalama Mkoa wa Shinyanga, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu Sabinus Chaula na Meneja Mkuu wa Mgodi wa Williamson Diamond Limited, Mhandisi Ayoub Mwenda.
Mkude amesema ziara hiyo imelenga kutaka kufahamu hatua gani zimefikiwa baada ya kupata janga la kubomoka kwa kingo za bwawa la Maji Tope katika Mgodi Almasi wa Mwadui tangu Novemba 7,2022 ikiwa ni miezi kadhaa sasa imepita.
“Leo nimefanya ziara ya kujiridhisha kwamba ni hatua gani zimefikiwa, Wenzetu wa Mgodi wa Williamson Diamond Limited wamechukua hatua mbalimbali kwanza za kuwanusuru wananchi waliokutwa na matope katika maeneo yao ya makazi na maeneo ya mashamba.
Hatua ya pili waliyofanya ni kuwapatia huduma zote muhimu wananchi waliothirika na janga hilo ikiwemo za afya, elimu kwa watoto waliokuwa wanasoma na kwa watu waliokosa makazi sasa hivi wote wamehifadhiwa kwenye nyumba za kupanga ambapo wamepangishiwa na Mgodi wa Mwadui mpaka hali yao itakapokuwa sawa wengine wanaendelea kupata huduma ya chakula tangu Novemba 7,2022”,ameeleza Mkude.
Amebainisha kuwa hatua zaidi zilizochukuliwa ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu la kutafuta eneo mbadala la kuishi ambalo ni salama kuliko lile wananchi walikuwa wanaishi ambapo eneo limepatikana katika kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge lenye ukubwa wa Hekari 400.
“Tumefika kwenye eneo hili na Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu ametueleza ukubwa wa eneo kuwa ni la hekari 400 ambazo kwa kweli wananchi walioathirika na tope zitawatosha wao makazi na kilimo kwa sababu eneo lina rutuba, lilikuwa eneo la serikali na halina mgogoro wowote”,amesema Mkude.
“Natumia fursa hii kuushukuru Mgodi wa Williamson Diamond Limited kwa kutimiza yale yote ambayo walielekezwa na serikali kwa kuweka miundo mbinu ya kuhifadhi maji tope yasizagae tena na mengine, lakini pia namshukuru Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kishapu kwa kutafuta eneo mbadala ambalo kwa kweli ni matumaini yangu hapa utaanza mji ambapo wananchi watapata huduma zote za msingi, shule zipo,kituo cha afya kipo, maji yapo, miundombinu ya barabara nitamsisitiza Mkurugenzi aiweke na umeme n.k”,ameongeza Mkude.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa