Madiwani Halmashauri ya wilaya ya Kishapu, wamelalamikia ubovu wa miundombinu ya barabara na Madaraja, na kusababisha baadhi ya Wajawazito kujifungulia njiani.
Wamebainisha hayo leo Januari 30, 2024 kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wakati wakiwasilisha taarifa za kwenye Kata zao na kubainisha changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili kubwa ikiwa ni ubovu wa miundombinu ya barabara na Madaraja.
Wamesema kutokana na Mvua ambazo zinaendelea kunyesha miundombinu mingi ya barabara imeharibika na Madaraja, hali ambayo imekata mawasiliano, huku Wajawazito wakipata tabu kwenda kwenye huduma za afya kujifungua pamoja na wanafunzi kupata shida wakati wa kwenda shule.
Mmoja wa Madiwani hao James Kasomi wa Kata ya Bubiki, amesema barabara ya kutoka Bubiki kwenda Bunambiu ni mbovu sana, na imesabasha Wajawazito Watano kujifungulia njiani wakati wakienda kujifungua katika Kituo cha Afya Bunambiu.
Naye Diwani wa Viti Maalumu Kata ya Bunambiu Helena Baraza amekazia ubovu wa Barabara hiyo, na kubainisha kuwa mwaka Jana kuna Mjamzito alijifungua kwenye daraja baada ya kushindwa kupita, na kusabisha mtoto kusombwa na maji na kupoteza maisha.
"Barabara hii ya kutoka Bubiki hadi Bunambiu ni mbovu sana, akina Mama Wajawazito wamekuwa wakipata tabu na wengine kujifungulia njiani, tunaomba ifanyiwe matengenezo sababu Mkandarasi ambaye alikuwa alikitengeneza haonekani," amesema Helena.
Madiwani hao kila mmoja alipokuwa akiwasilisha taarifa ya kwenye Kata yake changamoto kubwa ilikuwa ni ubovu wa Barabara, huku wengine walilalamikia ukosefu wa vyoo kwenye Magulio.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kishapu Francis Manyanda, amesema ni aibu akina Mama kujifungulia njiani bali Barabara hizo zifanyiwe matengenezo.
Kaimu Meneja Wakala wa Barabara Mjini na Vijjini (TARURA)wilayani Kishapu Mhandisi Hussein Shaweji, amesema ukarabati wa barabara hiyo upo kwenye utekelezaji, na Mkandarasi alianza na ujenzi wa Madaraja ijapokuwa kwa sasa amesimama sababu ya mvua kubwa kunyesha na mitambo kushindwa kupita.
Aidha, amesema kwa upande wa barabara zingine ambazo zimeharibiwa na Mvua, tayari wameshazifanyia tathimini na taarifa wameipeleka Makao Makuu, na wanasubiri kupatiwa fedha na kuanza kuzikarabati.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu Emmanuel Johnson, akijibu suala la Magulio kukosa vyoo, amesema Magulio yote ambayo Hayana vyoo yameshafungwa na hayafanyi kazi tena, ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu.
Amesema halmashauri hiyo imeshatenga fedha ya dharura kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vyoo kwenye Magulio yote yasiyo na vyoo, na wameshaanza na Magulio ya Nyasamba, Magalata,Mhunze na Sekeididi.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa