Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Christina Mndeme, amefanya ziara katika Mgodi wa Almasi Mwadui wilayani Kishapu, na kuagiza ujenzi wa bwawa jipya ambalo linajengwa kwenye Mgodi huo, lijengwe kwa kiwango cha juu ili kusijetokea tena ajali ya kupasuka na kuleta madhara kwa wananchi.
Novemba 7 mwaka jana (2022) bwawa la Mgodi wa Almasi Mwadui la kuhifadhi maji tope, lilipasuka kingo zake na kisha tope kuvamia makazi ya watu na kuleta madhara ya kupoteza mali zao, mashamba, nyumba kufunikwa, visima vya maji, lakini hakikutokea kifo hata kimoja.
Mdeme akizungumza katika ziara hiyo leo Mei 2,2023 amesema ametembelea Mgodi huo, ili kuona namna shughuli za uzalishaji madini hua zinafanyika,pamoja na kuona hatua ambayo wamefikia ya ujenzi wa bwawa jipya, na ulipaji fidia kwa wananchi.
"Katika ujenzi wa bwawa jipya ambalo mnaendelea kulijenga hivi sasa naagiza Mamlaka zote ambazo zinahusika wakiwamo NEMC, OSHA,Bonde mhakikishe linajengwa kwa kiwango cha juu ili kusije tokea ajali nyingine," amesema Mndeme.
"Bwawa hili likianza kutumika kuwe kunafanyika ukaguzi wa mara kwa mara pamoja na marekebisho ili kuchukua tahadhari na lenyewe lisije pasuka, mjifunze kutokana na makosa," ameongeza Mndeme.
Katika hatua nyingine Mndeme amewapongeza Mgodi huo kwa kulipa fidia wananchi ambao walipata madhara dhidi ya bwawa lililopasuka pamoja na kuwapatia huduma zote, huku akiagiza kwa wale 47 ambao watawajengea nyumba wazijenge nyumba za kisasa.
Aidha, amewataka wananchi ambao wanaishi jirani na Mgodi huo kuacha mara moja tabia ya kuvamia kwa ajili ya kuiba Mchanga wa madini, bali wafuate taratibu za kuomba Lesseni za uchimbaji na siyo kuvamia eneo la mwekezaji.
Naye Meneja wa Mgodi wa Almasi Mwadui Mhandisi Ayoub Mwenda, amesema tangu kupasuka kwa Bwawa la Mgodi huo la kuhifadhia Maji machafu wameshalipa fidia wananchi walioathirika asilimia 96, na mwezi June watawajengea nyumba waathirika 47 na pia waliopoteza mashamba watawafidia chakula.
Amesema katika hatua ambayo umefikia ujenzi wa bwawa jipya la kuhifadhia maji machafu ni asilimia 46 na hadi kufikia Julai mwaka huu litakuwa limekamilika, na Mwezi Agost ndipo wataanza Rasmi shughuli za uzalishaji wa Almasi.
Meneja ulinzi katika Mgodi huo Zephania Mwashitete, amesema Mgodi umeshajipanga kuimarisha suala la ulinzi, kwa kujenga uzio, kuweka CCTV kamera pamoja na Fiber wire ili kuzuia wananchi wasivamie ndani ya Mgodi huo.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa