Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack ameagiza wakurugenzi wa mamlaka za Serikali za Mitaa na Maji kuhakikisha hakuna mtu anayefanya shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo vya maji.
Telack alitoa agizo hilo juzi wilayani hapa katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese wakati wa kilele cha maadhimisho Wiki ya Maji yaliyofanyika kijiji cha Sekeididi.
Aliagiza wakurugenzi hao kuhakikisha vyanzo hivyo vinapandwa miti ili kutunza uoto wa asili ambao mara nyingi huathiriwa na ukame kutokana na kukosekana kwa miti.
Mkuu huyo wa mkoa aliwataka viongozi hao wasimamie utekelezaji wa sheria ya utunzaji wa mazingira ili kunusuru vyanzo vya maji, kwani Serikali inatumia fedha nyingi katika utekelezaji wa miradi ya maji.
“Utunzaji wa vyazo vya maji ni jambo muhimu katika upatikanaji wa maji na hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kutunza vyanzo vya maji kwa kupanda miti eneo linalozunguka vyanzo.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004, kifungu cha 57, kifungu kidogo cha 1 kinakataza mtu yeyote kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 60 kwenye vyanzo vya maji,” alisema.
Maadhimisho hayo yaliambatana na zoezi la upandaji miti kwenye bwawa la Sekeididi ambalo litakuwa likitoa huduma ya maji kwa wananchi wa maeneo hayo.
Telack aliwataka wananachi kuiunga mkono Serikali katika jitihada zake za kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo yao.
Na Ofisi ya Habari,Kishapu
Alisema miradi hiyo imeibuliwa na wananchi wenyewe kupitia vikao vyao na hivyo wanapaswa kuendeleza jitihada zao ili kunufaika nayo kwa kuwa wasimamizi wake.
Awali akizungumzia mradi wa ujenzi wa bwawa la maji kijijini hapo, Kaimu Mhandisi wa Maji Wilaya, Bernad Bwire alisema kuwa lina uwezo wa kuhifadhi lita milioni 119.8 za maji.
Alisema bwawa hilo linalojengwa kwa gharama ya sh. milioni 662.4 linatarajiwa kuhudumia wananchi 16,627 wa vijiji vinne vya Bugoro, Ngwashinong’ela na Mwagalankulu katika kata ya Sekebugoro.
Mhandishi Bwire alisema ili kulifanya bwawa lidumu wananchi wamejipanga kuhifadhi mazingira yanayolizunguka kwa kuzuia mifugo kuingia katika eneo la bwawa.
Aliongeza kuwa katika kipindi cha Wiki ya Maji jumla ya miti 230 imeshapandwa na kuwa wanatarajia kupanda mingine 800 zaidi katika eneo la kuzunguka bwawa hilo.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa