Shirika la Msaada na Mandeleo ya Jamii (REDESO) katika Halmashauri ya wilaya ya Kishapu limewapa mafunzo wazalishaji na wasindikaji wa zao la mkonge kutoka Kishapu na Meatu mkoani Simiyu.
Mafunzo hayo yaliyofanyika ukumbi wa Halmashauri Kishapu yanalenga kuwajengea washiriki hao uwezo wa utumiaji rasilimali kwa tija katika kuzalisha na kukidhi mahitaji ya soko la bidhaa wanazozalisha katika maeneo yao.
Mafunzo hayo yalitolewa kwa pamoja na Mshauri wa kujitegemea, Steven Tilubuza kutoka Mwanza na Afisa Ushirika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Stephano Shadrack.
Yanatarajiwa kuwapatia washiriki hao kutoka vikundi vya ujasiriamali elimu na ujuzi wa namna ya uanzishaji wa miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali kwenye maeneo hayo.
Meneja wa REDESO Kishapu, Charles Buregeya alisema washiriki hao kutoka vikundi vya ujasiriamali watanufaika na mafunzo hayo ambayo yatawajengea uwezo wa kutambua fursa mbalimbali waliko.
“Kupitia mafunzo hayo washiriki wataweza kujikwamua kutoka umaskini na kuwa na fursa nzuri za kujipatia kipato kwani wataweza kuibua na kuanzisha miradi ya maendeleo,” alisema Buregeya.
Pia aliongeza kwa kusema kuwa mafunzo hayo yatasaidia washiriki kupata elimu ya kubaini na kutafuta masoko ya bidhaa zao wanazozalisha hivyo kupata wigo mkubwa wa wateja.
Utaalamu mwingine washiriki wanaopata kupitia mafunzo hayo ni pamoja na namna ya ufungashaji mzuri wa bidhaa zilizozalishwa pia kuzitangaza kupitia njia mbalimbali ili ziwafikie wateja.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa