Na Ofisi ya Habari, Kishapu
Wananchi wa vijiji vya Mwajiginya A, Ubata na Mwaweja wilayani Kishapu mkoani Shinyanga wanatarajia kunufaika na mradi wa visima vya maji saba mwaka huu.
Hii ni baada ya kuwekwa jiwe la msingi ujenzi wa visima hivyo vyenye thamani ya sh. milioni 61.9 uliofadhiliwa na Shirika la Norwegian Church Aid-Tanzania (NCA) likishirikiana na TCRS pamoja na halmashauri ya Kishapu huku sh. milioni 1.6 zikiwa ni ndugu za wananchi.
Akizundua mradi huo, Diwani wa Kata ya Mwaweja, Makanasa Kishiwa alishukuru mashirika hayo kwa kuchangia shughuli za maendeleo na kuwataka wananchi waibue miradi ya maendeleo ili Serikali iwachangie.
Alisema wananchi wana jukumu la kuibua na kuanzisha miradi ili na Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo iwaunge mkono kwa kutekeleza miradi hiyo.
“Ninyi wananchi muibue miradi na Serikali itapeleka fedha kuikamilisha, haiwezi kutoa fedha kwa sehemu ambayo haina mradi hivyo nawaomba mchangamkie fursa hiyo,” alisema diwani.
Kishiwa aliongeza kwa kusisitiza kuwa sheria ziwabane wananchi wasiokuwa waaminifu wanaotumia muda wao kufanya uharibifu wa mazingira katika maeneo mbalimbali.
Ofisa miradi wa NCA, Zachayo Makobero alisema visima hivyo vitahudumia wananchi 2100 watakaopata maji ndani ya mita 400 kama sera ya maji inavyosema huku 9200 watapata huduma hiyo nje ya umbali wa mita hizo.
Alisema elimu ya utunzaji wa vyanzo vya maji na usafi wa mazingira kwa kata hiyo na zingine wilayani humo na vijiji vyake imeendela kutolewa ikiwa ni mwendelezo wa kampeni zilizofanyika mwaka jana.
Kwa upande wake, Mhandisi wa maji wilaya ya Kishapu, Lucas Said aliwataka wananchi kutunza vyanzo vya maji na kupanda miti ili kuepuka visikauke na kusababisha ukame.
Pia aliwataka kutunza miundombinu ya maji kwani imejengwa kwa gharama kubwa ili kuwahudumia huku akiizitaka kamati za maji vijijini kufanya kazi yake ipasavyo katika kuhudumia wananchi.
Mhandisi Said aliipongeza TCRS kwa kazi nzuri ya kuelimisha na kuhamasisha wananchi utunzaji mazingira na kuwataka wajenge na kutumia vyoo ili kuepuka maradhi.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa