WANAFUNZI 1,092,984 WALIOFAULU DARASA LA 7 WACHAGULIWA KUJIUNGA KIDATO CHA KWANZA 2024: WAZIRI MCHENGERWA.
Abainisha kuwa wanafunzi wote waliofaulu wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa Awamu Moja
Asema Bilioni 160 zimetolewa na serikali kujenga miundombinu ya Elimu 2022, Bilioni 140 zimetolewa 2023 Kukamilisha
Asema Bilioni 800 zimetolewa na Serikali kwa ajili ya kutoa Elimu bila Malipo nchini
Awataka MaRC na MaDC Kusimamia wanafunzi kuanza Masomo Januari 8, 2024 bila kuchelewa
Mhe. Mohamed Mchengerwa (Mb), Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI amesema Jumla ya wanafunzi 1,092,984 waliofaulu Mitihani ya Darasa la Saba wamechaguliwa kujiunga na Kidato cha Kwanza katika Shule mbalimbali za Sekondari nchini 2024 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi zaidi ya Elfu 16 sawa na 1.57% ukilingamisha na Mwaka 2023.
Waziri Mchengerwa amebainisha hayo mapema leo tarehe 17 Disemba, 2023 wakati wa Mkutano wake na wataalamu wa Sekta ya Elimu pamoja na waandishi wa habari uliofanyika kwenye Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza huku akibainisha kuwa ni 507,933 ni Wasichana na 585,051 wavulana.
Amebainisha kuwa kuwa uchaguzi wa wanafunzi umezingatia mambo mbalimbali kwa vigezo vya Ufaulu kulingana na kundi la shule huku akibainisha kuwa wanafunzi 5,606 wamepangiwa kwenye shule bora zaidi za bweni zipatazo 48 hapa nchini na kwamba 3,587 ni wenye Mahitaji Maalumu.
Ameongeza kuwa kutokana na uwepo wa Miundombinu bora na ya kutosha kwenye shule za sekondari nchini, wanafunzi wote waliogaulilu wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa Awamu Moja na kwamba wanafunzi wanaanza Masomo kwa Muhula unaoanza Januari 8, 2024 bila kuchelewa na Wakuu wa Mikoa na Wilaya Wasimamie hilo na kwamba taarifa zote za wanafunzi na fomu za kujiunga zinapatikana www.tamisemi.go.tz na www.necta.go.tz
"Kwa kutumia mifumo ya TEHAMA tumetekeleza kazi ya uchaguzi wa watoto hawa kwenda kwenye shule zetu kwa Uadilifu, Uaminifu na Uangalifu mkubwa sana tena kwa kuangalia Mgawanyo linganifu Kimikoa hususani kwa wale waliofaulu kwa juu zaidi na kupangiwa kwenda kwenye shule zetu pendwa" Dkt. Carles Msonde, Naibu K/M TAMISEMI anayeshughulikia Elimu.
Awali Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. CPA Amos Makalla alibainisha kuwa kwa kutekeleza kwa vitendo adhma ya Mhe. Rais ya kuwatumikia wananchi mkoa huo utatekeleza maagizo yote aliyoyatoa akiwa ndani ya ziara yake Mkoani humo hususani Wilayani Sengerema.
Amebainisha kuwa Viongozi wote Mkoani humo wapo imara kushirikiana katika kusimamia miradi ya maendeleo inayogharimu zaidi ya Bilioni 18 na kwamba itakamilika kwa wakati kadiri ilivyokusudiwa pamoja na ujenzi wa jengo la Abiria kwenye ujenzi wa Jengo la Kisasa la Uwanja wa Ndege wa Mwanza kuwa wa Kimataifa.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa