Waziri wa Madini Dotto Biteko amefanya ziara katika Mgodi wa uchimbaji madini ya Almasi Mwadui( Wiliamson Diamond LTD) uliopo wilayani Kishapu mkoani Shinyanga, na kuridhishwa na hatua ambayo imefikia ujenzi wa Bwawa jipya la kihifadhia Majitope na kuagiza uzalishaji wa Madini uanze Rasmi Julai 15 mwaka huu.
Mgodi huo wa Almasi Mwadui ulisimamisha shughuli za uzalishaji wa madini mara baada ya Bwawa lake la kuhifadhia Majitope kupasuka kingo zake Novemba 7 mwaka jana (2022)na kitiririka kwenye makazi ya wananchi na kusababisha madhara lakini hapakutokea vifo.
Biteko amefanya ziara hiyo leo Juni 30, 2023 akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali, kukagua hatua ambayo imefikia ujenzi wa Bwawa jipya la kuhifadhia Majitope ili kuanza shughuli za uzalishaji wa madini.
Amesema kwa maelezo ambayo amepewa pamoja na kujionea mwenye hatua ambayo imefikia ujenzi wa Bwawa hilo Jipya la kuhifadhia Majitope, ni vyema sasa shughuli za uzalishaji madini ya Almasi zikaanza, na hadi kufikia Julai 15 mwaka huu uzalishaji huo uwe umeshaanza, na Mkuu wa Mkoa atakwenda kuzindua Rasmi.
"Mgodi huu wa Almasi kusimamisha uzalishaji wa madini baada ya kutokea tatizo la kupasuka kwa Bwawa lake la Majitope Serikali imekosa mapato mengi sana, na Sekta ya Madini hapa nchini ndiyo inaongoza kwa kuingiza fedha za Kigeni, tunaka hadi Julai 15 muanze uzalishaji," amesema Biteko.
Katika hatua nyingine,ameuagiza Mgodi huo kukamilisha suala la ulipaji fidia kwa wananchi ambao wamesalia, ili kusiwepo na Malalamiko ya aina yoyote bali kila mtu aridhike na fidia ambayo amepewa.
Naye Mbunge wa Jimbo la Kishapu Boniphace Butondo, ameipongeza Serikali pamoja na Mgodi huo kwa hatua ambazo inaendelea kuzichukua tangu kupasuka kwa bwawa hilo, kwa kulipa fidia wananchi pamoja na kuwatimizia mahitaji yao yote tangu walipopatwa na maafa hayo.
Amesema kuanza kwa uzalishaji wa Madini katika Mgodi huo ni shauku kubwa kwa Wananchi wa Kishapu pamoja na Halmashauri kupata mapato, fedha ambazo zitatumika kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.
Naye Meneja Mkuu wa Mgodi wa Almasi Mwadui Mhandisi Ayoub Mwenda, amesema ujenzi wa Bwawa jipya la Majitope katika Mgodi huo limekamilika kwa asilimia 97,na lipo tayari kuanza kutumika na walikuwa wakisubili kupata vibari tu ilikuwasha mitambo.
Amesema kwa upande wa ulipaji fidia Wananchi, wameshalipa asilimia 96, na wameshashughulikia pia malalamiko ya wananchi 61 ambao walikuwa hawajaridhika na fidia na kusalia Watano.
Amesema pia ujenzi wa nyumba 47 za wananchi ambao walipoteza makazi yao, utaanza mwezi Julai kwa kujengewa nyumba hizo, huku fidia zingine za mashamba na upotevu wa vitu mbalimbali vya ndani wameshawalipa
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa