Mradi huu umegharimu jumla ya sh. bilioni 13.5 ambapo sh. bilioni 7.7 kati ya hizo zilitolewa na Serikali kupitia Wizara ya Maji na Umwagiliaji wakati wadau mbalimbali walichangia kiasi kilichobaki.
Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Kahama-Shinyanga (KASHWASA) ambayo ndiyo msambazaji mkuu ilipata mkopo wa kibiashara wenye riba sh. bilioni wakati Mgodi wa Almasi wa Mwadui wilayani Kishapu ilitoa mkopo usio na riba sh. bilioni 1.8.
Hivi sasa kwa wananchi wa wilaya hiyo changamoto ya uhaba wa maji imeweza kutatuliwa kwa asilimia kubwa hali inayoweza kuchangia kuendelea kuimarika kwa uchumi.
Kwa maji safi na salama yanayopatikana kutoka chanzo cha Ziwa Victoria sasa wananchi wanaweza kufanya shughuli za maendeleo tofauti na ilivyokuwa nyuma ambapo walikuwa wakitumia muda mwingi kusaka maji.
Idara ya Maji katika Halmashauri ya Wilaya Kishapu ikiongozwa na Mhandisi Lucas Said ambayo kwa sasa imezaa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira inaendesha mradi huo.
Awali ilikuwa ikisambaza maji kutoka chanzo kidogo cha maji kutoka Mto Tungu uliopo mjini Mhunze ambapo hata hivyo huduma hiyo ilikabiliwa na changamoto ikiwemo upungufu wa maji.
Kwa sasa baada ya kulifikisha bomba la maji kutoka chanzo cha ziwa hilo huduma ya maji imekuwa ya uhakika zaidi na saa za kufungulia maji zimeongezeka ikilinganishwa na awali.
Tayari tangi la maji lenye ujazo wa lita milioni 1.2 limeanza kujengwa ambalo linatarajiwa kukamilika mapema mwaka huu ambalo litakuwa likipokea maji ya Ziwa Victoria na kuyasambaza katika Mji wa Mhunze na vitongoji vyake.
Mwishoni mwa mwaka 2016, Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhandisi Gerson Lwenge aliweka Jiwe la Msingi kwenye mradi wa ujenzi wa tangi hilo eneo la Mhunze ikiwa ni sehemu ya upanuzi wa mradi huo.
Utekelezaji wa awamu ya kwanza ulianza rasmi Februari 2015 kutokana na mkopo kutoka Benki ya CRDB baada ya kukamilika kwa mchakato wa ununuzi wa bomba na viungio.
Hata hivyo, kuanzia Aprili hadi Mei 2015 ujenzi ulisimama kutokana na mvua kubwa zilizokuwa zikinyesha kwa kipindi hicho. Ujenzi ulianza tena Mei na kukamilika Desemba mwaka huo.
Changamoto nyingine zilizochangia uchelewaji wa mradi ni ongezeko la kazi mpya ya ulipuaji wa miamba kwenye njia ya bomba, uwepo wa mawe mengi kwenye mtaro wa bomba hali iliyolazimisha kutumia mchanga kutoka maeneo mengine kabla ya kulaza.
Awamu ya pili ilianza Mei 2016 na kuchelewa kuanza kwa utekelezaji wake kulitokana na changamoto ya upatikanaji wa fedha kutoka Wizara ya Maji na Umwagiliaji.
Usanifu wa awali uliofanywa na Kampuni ya GIBB East Africa ulionesha kwamba bomba kuu la kusafirisha maji kwenda Kishapu lingeunganishwa kwenye tangi kubwa lililopo eneo la Old Shinyanga linalotumiwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Shinyanga (SHUWASA).
Bomba hilo, lingepitia eneo la Kolandoto na vijiji mbalimbali hadi katika Mji wa Kishapu. Aidha, Mgodi wa Almasi wa Mwadui nao ungeunganishwa kwa bomba dogo karibu na Kolandoto.
Pia, usanifu ulionesha kwamba katika eneo hilo kingejengwa kituo cha kuongeza Msukumo wa maji ‘booster station’ ili kuwezesha maji kufika Kishapu.
Njia ya bomba ilibadilishwa ili ipitie Maganzo badala ya Kolandoto kupunguza umbali wa kufikisha maji Mwadui na vijiji vyote vilivyojumuishwa kwenye usanifu ambavyo ni Ihapa, Ikonongo, Utemini, Nyenze, Ukenyenge, Mayanji, Negezi, Uchunga, Wela, Ngundangali, Kakola, Unyanyembe na Mwamashele.
Eneo la kujenga tangi katika Mji wa Kishapu lilibadilishwa kutoka kwenye eneo la awali kwenda eneo jipya lenye mwinuko mkubwa zaidi, ikilinganishwa na eneo la awali. Aidha, kwa kutumia eneo jipya, urefu wa njia ya bomba unapungua.
Halmashauri ya Wilaya Kishapu
Anwani ya Posta: S.L.P. 1288 KISHAPU
Simu ya mezani: +255282770020
Simu:
Barua pepe: info@kishapudc.go.tz/ded.kishapudc@shinyanga.go.tz
Hakimiliki © 2016 Halmashauri ya wilaya ya Kishapu. Haki zote zimehifadhiwa